Kwa muda mrefu kabla ya Mungu kuwaumba watu, Mungu aliwaumba malaika wengi sana ambao waliishi naye mbinguni. Aliwaumba wazuri bila dhambi, na pia walikuwa roho. Malaika walimwabudu Mungu na walikuwa watumishi wake pia.
Malaika mmoja fulani aliyeumbwa na Mungu alikuwa mwerevu na mrembo kuliko malaika wengine wote. Malaika huyo aliitwa Lusifa. Mungu alimpatia Lusifa mamlaka juu ya malaika wengine wote.
Baada ya muda fulani, Lusifa akawa na kiburi sana, akaamua awe muhimu na wa maana kama Mungu. Akataka kuingia mahali pa Mungu. Malaika wengine wengi pia waliamua kuasi dhidi ya Mungu. Lakini Mungu alijua Lusifa na malaika wengine walivyofikiri. Maasi yao yalishindwa kwa maana Mungu anajua kila kitu na ni mwenye nguvu kuliko Lusifa aliyeumbwa na Mungu mwenyewe.
Kwa sababu ya dhambi ya Lusifa na malaika wake, Mungu aliwafukuza kutoka mbinguni walipokuwa wakiishi pamoja naye. Mungu ni mwenye haki na ni mtakatifu kwa hivyo hangeweza kuishi pamoja na walioasi mbele yake. Mungu pia alisema kwamba siku moja atakamilisha adhabu yake kwa malaika waasi na kuwatupa katika Ziwa la Moto.
Mungu alibadilisha jina la Lusifa kuwa Shetani. Jina hilo linamaanisha “Mdanganyifu.” Kwa hivyo Shetani na wafuasi wake wakawa maadui wa Mungu. Wao hupinga kazi ya Mungu wakati wote.
Sasa wafuasi wa Shetani ni mapepo waovu. Wao hufuata Shetani kupinga ukweli.
Shetani hataki tusikilize Neno la Mungu. Lakini wanaomwamini Mungu hawahitaji kumwogopa Shetani au mapepo yake kwa sababu Mungu ana nguvu juu ya wote.